Tuesday, January 8, 2013

OMAR OMAR MFALME WA MNANDA BONGO KUZIKWA KESHO MIKOROSHINI


Omar Omar

MSANII nyota wa miondoko ya Mchiriku, Omari Omari, aliyefariki leo afajiri atazikwa kesho saa 7 mchana.
Kwa mujibu wa King Sapeto, rafiki wa karibu wa marehemu, mazishi yatafanyika Temeke Mikoroshini jijini Dar es Salaam na kuanzia leo ndugu na jamaa wa marehemu wanategemea ujumbe mzito kutoka kwa viongozi wa Serikali watakaopishana kwenda kutoa mkono wa faraja kwenye nyumba ya msiba.
Kwa siku za hivi karibuni viongozi wa serikali na vyama mbali mbali vya siasa wamekuwa mstari wa mbele kwa kushiriki bega kwa bega kwenye misiba ya wasanii, hivyo watu wa karibu na Omari Omari wanategemea hali hiyo pia itatokea kwa ndugu yao kipenzi. "Hatutegemi ubaguzi wa misiba" anaeleza mmoja wa ndugu wa marehemu.
Omari Omari aliyetamba na wimbo “Kupata Majaaliwa” ndani yake kukiwa na mstari mkali unaosema ndefu amekosa ng’ombe lakini mbuzi kapewa, alifariki katika hospitali kuu ya Temeke baada ya kuugua ugonjwa wa kifua kikuu. Msiba uko Temeke Mikoroshini nyumbani kwa baba yake.

No comments:

Post a Comment