Sunday, January 20, 2013

STEWART AJIVUNIA KIWANGO AZAM LICHA YA KIPIGO KENYA JANA


Azam katika mechi ya jana
LICHA ya kupoteza mchezo wake wa kwanza wa kirafiki dhidi ya AFC Leopard jana, kocha wa Azam FC Stewart Hall amesema timu yake imecheza vizuri na kufungwa ni sehemu ya mchezo.
Stewart alisema haikuwa bahati kwao kwa kuwa walipata nafasi nyingi za wazi umaliziaji ukawa tatizo, pia na penati mbili walizopata wachezaji wake walikosa na kuipa ushindi timu hiyo iliyokuwa na mashabiki wengi uwanjani hapo.
“Timu inayocheza vizuri ni ile inayotengeneza nafasi na kucheza mpira mzuri, tulicheza vizuri nafurahi kuona wachezaji wanajituma, kukosa penati na nafasi za wazi ni matatizo yanaweza kuzibika” alisema Stewart.
Aliongeza kuwa kupitia mechi hizi zote watakuwa na wakati mzuri wa kurekebisha makosa yanayotokea kabla ya kuanza kwa mechi za ligi.
Katika mchezo huo AFC Leopards walikuwa wa kwanza kupata magoli yalifungwa katika dk ya 14 na Paul Were na dk 54 Mike Baraza aliifungia timu hiyo goli la pili kufuatia kosa la beki wa Azam FC, kumruhusu akapiga shuti likaenda moja kwa moja wavuni.
Azam FC walipata penati tatu katika dk 19, Jockins Atudo alikosa baada ya kupiga mkwaju uliotoka nje, dk 65 Khamis Mcha nae alikosa penati baada ya kugonga mwamba na kurudi ndani ikaokolewa na mabeki wa AFC.
Goli la Azam FC lilipatikana kupitia kwa mkwaju wa penati iliyopigwa na Samih Haji Nuhu baada ya beki wa AFC Erick Masika kumwangusha Humprey Mieno kwenye eneo la hatari.
Kipindi cha pili Kocha Stewart alifanya mabadiliko walitoka, Luckson Kakolaki, Salum Abubakar, Abdulhalim Humud, Uhuru Seleman, Jabir Aziz na Gaudence Mwaikimba nafasi zao zikachukuliwa na David Mwantika, Michael Bolou,Humphrey Mieno, Ibrahim Mwaipopo, Brian Umony na Abdi Kassim, mabadiliko hayo yaliimarisha kikosi hicho muda wote wa mchezo.
Baada ya mchezo huo kocha wa AFC, Tom Olaba alisema kupata ushindi kwa kuifunga timu bora ni mafanikio kwake na kuonyesha ukomavu kwa wachezaji wake.

No comments:

Post a Comment