Tuesday, December 25, 2012

HASANOOO ALIA BATA JELA -XMASS HIII !!!


Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam,  imezuia dhamana dhidi ya kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoani Pwani (Corefa), Hassani Othman maarufu kama Hasanoo (43) ya mashtaka matatu likiwemo la kuhujumu uchumi na kusafirisha pembe za ndovu zenye thamani ya Sh. bilioni 1.1kutoka Dar es Salaam kwenda Hong Kong kutokana na kutenda kosa hilo akiwa nje kwa dhamana ya kesi nyingine ya wizi wa tani 26 za madini ya shaba yenye thamani ya Sh. milioni 400.

Hata hivyo, mahakama hiyo imekubali kutoa masharti ya dhamana kwa washtakiwa wengine sita ambao ni Ally Kimwaga, Dunstan Mwanga, Godfrey Mwanga, John Mlai, Khalid Fazaldin na Lusekelo Mwakajila.
 Uamuzi huo ulitolewa  na Jaji Zainabu Mruke baada ya kusikiliza hoja za mawakili wa pande zote mbili.

Alisema kipengele cha 36, kifungu kidogo cha (4) kidogo (c) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi, kinaeleza wazi kwamba sheria inaifunga mikono mahakama kuhusu maombi ya dhamana kwa mshtakiwa wa kwanza ambaye amekutwa na tuhuma za uhujumu uchumi akiwa nje kwa dhamana ya kesi nyingine inayomkabili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

“Kutokana na sababu hiyo, mahakama haiwezi kutoa dhamana kwa mashtakiwa wa kwanza (Hasanoo) kwani amekutwa na tuhuma za uhujumu uchumi wakati akiwa nje kwa dhamana… mahakama inanifunga mimi kama Jaji kwa mujibu wa kipengele cha 36 kidogo cha (4) na kidogo (c) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi, hakuna dhamana kwa mshtakiwa huyo,” alisema Jaji Mruke.

Alisema mshtakiwa wa pili hadi wa saba, mahakama hiyo imeona wana haki ya kisheria kupata dhamana kwa kufuata masharti yatakayowekwa na mahakama.

Jaji Mruke aliyataja masharti hayo kuwa ni kuwasilisha hatia zao za kusafiria kwa Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam na kwamba, hawaruhusiwi kutoka nje ya mkoa wa Dar es Salaam bila kibali cha msajili huyo hadi kesi yao ya msingi itakapomalizika.

Alisema vilevile kuwa mshtakiwa wa pili hadi wa saba wajidhamini kwa Sh. milioni 50 au kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo ya fedha.

“Nakala zote za masharti ya dhamana ziwasilishwe katika Mahakama ya Kisutu inakosikilizwa kesi hii ili kuondoa mkanganyiko” alisema Jaji Mruke.

Baada ya uamuzi huo kusomwa, wanaodaiwa kuwa ndugu wa Hasanoo waliangua kilio kutokana vifungu vya sheria kumbana ndugu kutoka nje kwa dhamana. Uamuzi huo pia ulimaanisha kuwa Hassanoo atakuwa mahabusu katika kipindi chote cha sikukuu za mwisho wa mwaka, ikiwamo ya krismasi (X-Mass) inayosherehekewa leo.

Ijumaa iliyopita katika mahakama hiyo, mawakili wa utetezi Richard Rweyongeza, Majura Magafu, Aliko Mwamanenge, Pascal Chuwa na Charles Semgalawa, kwa nyakati tofauti waliwasilisha hoja za kuwaombea dhamana washitakiwa.

Katika kesi ya msingi, washitakiwa wanakabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la uhujumu uchumi na kusafirisha meno ya tembo, yenye thamani ya Sh.bilioni 1.1 kwenda Hong Kong nchini China.

Ilidaiwa kuwa katika shtaka la kwanza, washtakiwa walikula njama na kujihusisha katika biashara ya kusafirisha nyara za Serikali bila leseni, kosa ambalo walilitenda kati ya Septemba Mosi na Novemba 20, mwaka huu, Dar es Salaam na Hong Kong kinyume na kifungu cha 384 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.

No comments:

Post a Comment