Saturday, October 20, 2012

SAMATTA, ULIMWENGU KUIBEBA MAZEMBE LEO TUNISIA?

Samatta ataibeba Mazembe leo?

TOUT Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) leo ina mtihani mgumu mbele ya Esperance ya Tunisia katika mchezo wa marudiano wa Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika mjini Tunis.
 
 
Hiyo inatokana na Mazembe kulazimishwa sare ya bila kufungana na mabingwa hao wa Afrika, katika mchezo wa kwanza kwenye Uwanja wa Stade du TP Mazembe mjini Lubumbashi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wiki mbili zilizopita.
 
 
Sare yoyote ya mabao inaweza kuivusha Mazembe hadi fainali, lakini Esperance inapewa nafasi kubwa ya kushinda kwa kuwa itakuwa ikicheza nyumbani.
 
Mchezo huo tayari umekuwa gumzo kubwa, kutokana na upinzani mkubwa baina ya timu hiyo na hasa baada ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF), kubadilisha refa wa mechi hiyo siku tatu kabla ya timu hizo kurudiana.
 
CAF imeteua marefa wapya wa kuchezesha mechi hiyo ya leo kufuatia malalamiko yaliyowasilishwa na Mazembe dhidi ya refa Bakary Gassama kutoka Gambia na sasa Badara Diatta wa Senegal ndiye ambaye sasa atachezesha mechi hiyo mjini Tunis.
 
Magazeti nchini Tunisia yamepinga uteuzi wa refa mpya kwa sababu anatoka nchi moja na kocha wa Mazembe, Lamine N’Diaye, ambaye ni Msenegal pia.
 
 
Mazembe ina washambuliaji hatari wa Kitanzania, Mbwana Ally Samatta na Thomas Emmanuel Ulimwengu ambao wote kwa sasa ni tegemeo la timu hiyo.
 
 
Katika mchezo wa leo, Mazembe itamkosa beki wake tegemeo, Stopila Sunzu aliyepewa kadi ya pili ya njano (nyekundu) dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 90 za kawaida kwenye mechi ya kwanza.
 
 
Awali, Sunzu kaka wa mshambuliaji wa Simba, Felix Sunzu, alionyeshwa kadi ya kwanza ya njano dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha kwanza.
 
 
Washambuliaji wote wawili wa Kitanzania walicheza mechi hiyo, Mbwana Ally Samatta alicheza hadi dakika 83 alipompisha Sinkala, wakati Thomas Emanuel Ulimwengu alitokea benchi dakika ya 58 kwenda kuchukua nafasi ya D. Kanda.
Nusu Fainali nyingine ya michuano hiyo inatarajiwa kuchezwa kesho kati ya mabingwa mara sita Afrika, Al Ahly ya Misri na Sunshine Stars ya Nigeria mjini Cairo. Katika mechi ya kwanza ya iliyopigwa huko Ijebu-Ode kwenye Uwanja wa kimataifa wa Dipo Dina, timu hizo zilitoka sare ya kufungana mabao 3-3.
 
 
Nahodha wa Sunshine, Godfrey Oboabona aliikosa mechi hiyo baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano katika mechi ya mwisho ya makundi dhidi ya Esperance ya Tunisia, wakati Mohamed Aboutrika alikuwa anatumikia adhabu ya kufungiwa miezi miwili na Ahly.
 
 
Ahly ilipata bao la kwanza dakika ya 18 kupitia kwa Mohamed Nagy, aliyefumua shuti kutoka nje ya boksi na kumtungua Moses Ocheje, kabla ya Mahdy El Sayed kuifungia bao la pili timu hiyo dakika ya 30, wakati Sunshine ilipata bao la kwanza dakika ya 40, kupitia kwa kiungo Mcameroon, Tamen Medrano aliyemtungua kwa shuti la mbali kipa wa Ahly, Sherif Elkramy.
 
 
Wenyeji walisawazisha dakika ya 73 kwa mkwaju wa penalti wa Dele Olorundare baada ya Ajani Ibrahim kuangushwa kwenye eneo la hatari na Mohamed Nagy.
Pamoja na hayo, Mashetani Wekundu wa Cairo walipata bao lililoelekea kuwa la ushindi, dakika moja badaaye kupitia kwa kijana mwenye umri wa miaka 25, Nagy ambalo lilikuwa bao lake la pili kwenye mechi hiyo.
 
 
Beki wa Sunshine, Precious Osasco aliisawazishia timu yake dakika ya 83 kwa shuti la mpira wa adhabu lililomshinda kipa Elkramy.  Nagy alipata nafasi ya kukamilisha hat-trick dakika tatu kabla ya filimbi ya mwisho, lakini kichwa chake kiliupaisha mpira alipokuwa anaunganisha kona. 

SIMBA SC TAYARI WENYEJI TANGA, KAPOMBE, BOBAN, NYOSSO WAACHWA DAR

Simba SC

MABINGWA watetezi, Simba SC tayari wako mjini Tanga tangu jana jioni kwa ajili ya mechi yao ya kesho dhidi ya wenyeji JKT Mgambo katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
 
 
Simba iliyoanza Ligi Kuu kwa kishindo, ikishinda mechi sita mfululizo, imelazimishwa sare katika mbili mfululizo zilizopita 0-0 na Coastal Union mjini Tanga na 2-2 na Kegara Sugar mjini Dar es Salaam na 
 kesho imepania kumaliza mduduwa sare.
 
 
Kocha Mserbia, Profesa Milovan Cirkovick amesema yeye na wachezaji wake wamejifunza jambo baada ya sare ya pili na Kagera Jumatano na sasa wataongeza juhudi zaidi ili kuhakikisha matokeo hayo hayajirudii.
 
 
Lakini Mgambo nayo, iliyoanza Ligi kizembe, imezinduka na kushinda mechi tatu mfululizo, tena moja ya ugenini dhidi ya Mtibwa Sugar 2-1 wiki iliyopita kabla ya kushinda 2-0 dhidi ya Toto African mjini Tanga.   
 
 
Simba imeenda Tanga na wachezaji wake 24, ambao ni makipa; Juma Kaseja Juma, Wilbert Mweta William na Waziri Hamad Mwinyiamani, mabeki Nassor Said Masoud ‘Chollo’, Amir Maftah Mrisho, Paulo George Ngalema, Koman Bili Keita, Pascal Ochieng Akullo, Hassan Hatibu Kondo.
 
 
Viungo ni Jonas Mkude Gerrald, Ramadhani Chombo Redondo, Amri Kiemba Athumani, Abdallah Omar Seseme, Ramadhani Singano Yahya, Uhuru Selemani Mwambungu, Mrisho Khalfan Ngassa, Mwinyi Kazimoto Mwetula na Salim Abdallah Kinje na washambuliaji Abdallah Juma, Daniel Akuffo, Felix Mumba Sunzu, Edward Christopher Shija, Haruna Athumani Chanongo na Emmanuel Arnold Okwi.
 
 
Waliobaki Dar es Salaam ni Haruna Moshi ‘Boban’ anayesumbuliwa na maumivu ya misuli, Haruna Shamte, anayeumwa goti, Kigi Makassy anayeumwa goti pia, Shomari Kapombe anayesumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu na Juma Said Nyosso anayetumikia adhabu ya kadi (tatu za njano).
 
 
Simba bado inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 18, baada ya kucheza mechi nane, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 17, baada ya kucheza mechi saba, wakati Yanga inayocheza mechi ya nane na Ruvu Shooting leo Dar es Salaam ni ya tatu kwa pointi zake 11.   

No comments:

Post a Comment