Sunday, September 30, 2012

Sunday, September 30, 2012

VODACOM BADO IPO IPO SANA LIGI KUU BARA

Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa

BAADA ya kikao cha pamoja cha majadiliano kati ya Mdhamini mkuu wa Ligi Kuu Vodacom Tanzania Bara, Kamati ya ligi, TFF na klabu zinazoshiriki ligi hiyo, mashabiki na wapenzi wa soka nchini wameondolewa hofu juu ya udhamini wa ligi inayoendelea hivi sasa.
 
Mdhamini mkuu wa ligi hiyo Vodacom Tanzania, imekubali kuendelea kuunga mkono ligi hiyo na kuwaomba mashabiki wa soka kutegemea msimu mzuri wa ligi mwaka huu.
 
Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa, amesema kuwa mvutano ambao umekuwepo baina ya baadhi ya Vilabu vya soka na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) pamoja na wadhamini sasa yamepatiwa ufumbuzi.
 
“Kulikuwa na sinto fahamu kati ya Klabu za ligi kuu TFF na sisi kama wadhamini, tulikaa kikao siku ya ijumaa na wadau wote wa ligi na sasa mambo yote yamewekwa katika msitari,” alisema Kelvin na kuongeza kuwa “ Tumedhamiria kuendelea kuiunga mkono Ligi kuu ya Vodacom hatukuwa na matatizo yoyote katika kusaini mkataba na kamati ya ligi ni ufafanuzi tu ndio ulihitajika  ili kuwekana sawa,” alisema Twissa.
 
Kuhusiana na kutolewa kwa fedha za udhamini na uendeshaji wa ligi na udhamini wa kampuni pinzania twissa alisema Vodacom haizuii klabu za ligi kudhaminiwa na kampuni nyingine yoyote tofauti na zile zenye msingi wa kiushindani katika biashara na kampuni hiyo.
 
“Kufuatia kikao hicho na kuwa katika msitari mmoja tumekwisha toa fedha na vifaa kwa TFF na vilabu ili ligi iweze kwenda kama ilivyo takiwa,Tukiwa kama wadau katika kuunga mkono maendeleo ya soka nchini, tumeruhusu kampuni nyingine ambazo hazina upinzani wa kibiashara na sisi ili kuondoa muingiliano wa kimaslahi,” alisema.
 
“TFF inadhamana ya kusimamia sheria na masharti kuhusu ligi. Hatuna matatizo yoyote ya kiutendaji na TFF wala klabu yoyote” alihitimisha Twissa.
 
Ligi kuu ya Vodacom ilianza rasmi tarehe 15  mwezi septemba, na tutashuhudia michezo 182 kwa kushirikisha timu 14 zinazoshiriki katika ligi hiyo, zikiwemo Yanga Afrika, Kagera sugar, na Simba ambaye ndie bingwa mtetezi wa ligi kuu ya Vodacom.
 
Kampuni ya Vodacom imekuwa mdhamini wa ligi kuu kwa miaka mitano sasa, na imesaini mkataba mpya wa udhamini wa ligi hiyo kwa miaka mitatu na shirikisho la mpira wa miguu TFF, mkataba utakao shuhudia shirikisho hilo likipokea udhamini wa kila msimu kwa miaka mitatu mfululizo.

 

 

SIMBA WAKIPIGA NA ZANZIBAR ALL STARS LEO USIKU AMAAN

kutoka kushoto waliosimama ni emanuel okwi,juma nyoso,haruna moshi boban,amri kiemba ,daniel akuffor,na juma kaseja ,,,na walioinama kutoka kushoto ni said nassoro,mwinyi kazimoto,,amir maftah,,salum kinje na shommari kapombe wachezaji hawa wa Simba SC


SIMBA SC inatarajiwa kushuka dimbani kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar kuanzia saa 2:00 leo kumenyana na All Stars ya Zanzibar katika mchezo wa kirafiki, kujiandaa na mpambano dhidi ya watani wao wa jadi, Yanga Jumatano, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 
Simba imerejea leo Zanzibar, baada ya jana kuendeleza wimbi lake la ushindi katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kwa kuichapa Prisons ya Mbeya iliyorejea Ligi Kuu msimu huu mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 
Mabao ya Simba yalitiwa kimiani na Felix Mumba Sunzu na Mrisho Ngassa, ambaye hilo ni bao lake la kwanza katika Ligi Kuu ndani ya mechi nne na la pili jumla tangu ajiunge na timu hiyo katika mechi saba alizocheza, wakati la Prisons lilifungwa na Elias Maguri.
 
Kwa ushindi huo, Simba imefikisha pointi 12 na kurejea kileleni mwa Ligi Kuu, ikiizidi Azam FC pointi mbili katika nafasi ya pili, ingawa timu zote zimecheza mechi sawa, nne.
 
Hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zikwishafungana bao 1-1, Prisons wakitangulia kupata bao dakika ya sita baada ya Maguri kuwatoka mabeki wa Simba kupiga shuti lililomgonga Shomary Kapombe na mpira kupoteza mwelekeo na kumchanganya kipa na Nahodha wa Simba, Juma Kaseja na kutinga nyavuni.
 
Baada ya bao hilo, timu hizo ziliendelea kushambuliana kwa zamu, ingawa Prisons waliendelea kuwa wagumu, hadi walipojisahau kidogo sekunde za mwishoni za kipindi cha kwanza na Felix Sunzu akatumia pasi ya Amiri Maftah kusawazisha dakika ya 45.
 
Kipindi cha pili, Simba walirudi na moto na kuanza moja kwa moja kulishambulia mfululizo lango la Prisons na dakika ya 55 Ngassa akafunga kwa shuti dhaifu, ambalo kipa wa Prisons, David Abdallah alidaka lakini mpira ukamtoka na kuingia nyavuni.
 
Mechi hiyo ilichezeshwa na refa, Paul Soleji kutoka Mwanza, aliyesaidiwa na Jesse Erasmo, mshika kibendera namba moja, Mwarabu Mumba mshika kibendera namba mbili, wote kutoka Morogoro, wakati refa wa Akiba alikuwa Israel Nkongo wa Dar es Salaam. 
 
Dakika ya 87 Amir Maftah alipewa kadi nyekundu kwa kumchezea rafu Khalid Fupi wa Prisons, hivyo ataukosa mchezo ujao dhidi ya Yanga Jumatano na hiyo ni nafasi kwa chipukizi Paul Ngalema.
 
Hiyo inakuwa kadi ya pili nyekundu kwa Simba ndani ya mechi nne, awali katika mechi ya pili dhidi ya JKT Ruvu, Emmanuel Okwi alilimwa kadi ya aina hiyo kwa kumpiga kiwiko Kessy Mapande na akafungiwa mechi tatu.
 
Kikosi cha Simba jana kilikuwa; Juma Kaseja, Nassor Masoud ‘Chollo’, Amir Maftah, Shomari Kapombe, Juma Nyosso, Mwinyi Kazimoto, Amri Kiemba/Salim Kinje, Ramadhan Chombo/Jonas Mkude, Christopher Edward/Daniel Akuffo, Felix Sunzu na mrisho Ngassa.
 
Prisons: 18.David Abdallah, 03.Aziz Sibo, 05.Laurian Mpalile, 16.Lugano Mwangama (Nahodha), 15.David Mwantika, 13.Khalid Fupi, 07.Misango Magai, 12.Fred Chudu/22.Julius Kwaga, 14.Elias Maguri, 17.Peter Michael/Sino Augustino na 19.John Matei/11.Hamisi Ally.

No comments:

Post a Comment