Thursday, January 10, 2013

CHAMA CHA NGUMI ZA KULIPWA AFRIKA MASHARIKI NA KATI ECAPBA YATEUA WAAMUZI


Chama Cha Ngumi za Kulipwa Cha Afrika ya Mashariki na Kati (ECAPBA) kinachoratibu ubingwa wa ECAPBF kimewateua waamuzi wa mpambano kati ya Mtanzania Thomas Mashali na bondia Bernard Mackoliech kutoka nchini Kenya.

Mpambano huo ni wa kutetea ubingwa wa ECAPBF uzito wa Middle ambao Thomas Mashali aliupata baada ya kumsambaratisha bondia Med Sebyala kutoa nchini Uganda mwaka jana.

Akitangaza waamuzi hao, Rais wa ECAPBA Onesmo Ngowi alisema kuwa Mark Hatia atakuwa msimamizi mkuu wa pambano hilo. Nemes Kavishe ambaye ndiye Mweka Hazina wa ECAPBA atakuwa ndiye refarii wa mpambano huo. Majaji watatu watakuwa ni Fidel Haynes, Said Chaku na Sakwe Mtulya.

Mpambano huo utafanyikia wakati wa sikukuu ya Mapinduzi ya Zanzibar katika ukumbi wa Friends Corner, wilaya ya Kinondoni, jijini Dar-Es-Salaam.

Katika hatua nyingine, ECAPBA inajiandaa kuhamia katika jiji la Arusha baada ya kuombwa na uongozi wa jiji hilo kuhamishia makao yake makuu ili kuwa karibu na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC).

Juhudi za ECAPBA kuhamia Arusha zinafanywa na Meya wa jiji hilo, Mstahiki Gaudence Lyimo ambaye ni mpenzi wa michezo na maendeleo ya vijana.

No comments:

Post a Comment